Monday , 29th Feb , 2016

Serikali imesema kuwa italazimika kuivunja halmashauri ya Tanga endapo mgogoro wa kisiasa wa Halmashauri hiyo hautamalizika kutokana na kushindwa kukaa na kufanya vikao vya maendeleo.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza na viongozi wa serikali na kisiasa Jijini Tanga jana Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan amesema kuwa mpaka sasa hakuna uongozi unaosimamia maendeleo ya wananchi kutokana na mgogoro huo ambao unahusisha Chama cha Mapinduzi na Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi(UKAWA).

Mhe. Samia ameongeza kuwa wananchi wanahitaji maendeleo na serikali haitaweza kuruhusu kurudia uchaguzi katika halmashauri hiyo kutokana na gharama hivyo itabidi kuweka uongozi wa mpito mpaka hapo uchaguzi mwingine wa kikatiba utakapofikia.

Aidha Makamu huyo wa Rais ameongeza kuwa Jiji la Tanga lipo hatarini kuondolewa katika mipango ya maendeleo ikiwemo na kukosa fursa ya kujengewa viwanda hivyo hawana budi kukaa pamoja viongozi wote wa halmashauri hiyo ili kutatua tatizo hilo.