Jumanne , 2nd Dec , 2025

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa wito wa amani na uvumilivu kwa Watanzania wote, akiwataka Viongozi wa Dini na wananchi kwa ujumla kuepuka maneno na matendo yanayoweza kuvuruga utulivu wa nchi.

 

Akizungumza na Wazee wa Dar es Salaam leo, Desemba 2, 2025, Dkt. Samia amesema kwamba hata kama mtu hampendi yeye binafsi, ni vyema kuvumilia hadi amalize muda wake badala ya kuchochea vurugu.  

“Hata kama haumpendi Rais, vumilia tu... ataondoka. Wote waliotangulia waliiongoza nchi kwa amani. Kwa nini leo tufarakane kwa sababu ya chuki binafsi au tofauti za dini?” alisema Rais Samia.

Ameonya dhidi ya matumizi ya dini kama silaha ya kuchochea chuki na migawanyiko, akiwataka viongozi wa dini kuwa mfano wa kuigwa kwa kuhubiri upendo, mshikamano na kuheshimu mamlaka.

Rais Samia pia alisisitiza kuwa mafanikio ya serikali ya awamu ya sita yameonekana katika sekta mbalimbali kama afya, elimu na uchumi – akitoa wito kwa wananchi kutumia akili zao badala ya kuendeshwa na propaganda za kisiasa.