Alhamisi , 15th Aug , 2024

Tanzania inatarajiwa kuongeza umeme wa  Kilowati 360 katika gridi ya Taifa endapo umeme unaozalishwa kwa njia ya maporomoko ya maji ya Ijangala uliopo Wilaya ya Makete, Mkoa wa Njombe utakamilika kwa wakati

 

Kauli hiyo imetolewa baada ya bodi ya Nishati Vijijini kutembelea na kukagua mradi wa kuzalisha umeme kwa njia ya maporomoko hayo na kuahidi kuendelea kuwawezesha waendelezaji binafsi wa umeme nchini.

Akizungumza mara baada ya kutembelea mradi huo, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi Meja Jenerali (mstaafu), Jacob Kingu amepongeza uanzishwaji wa mradi huo ambapo kukamilika kwake kutaongeza wingi wa umeme nchini 

“Sisi kama Bodi ya Nishati Vijijini mara hii tulipanga kufanya kikao chetu cha Bodi Njombe ambapo tunamiradi inayoendelea ili kuona uhalisia wakati tunajadili na kujionea miradi hiyo inayoendelea na changamoto zake ili kuwa katika nafasi nzuri ya kuijadili na kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinayoikabili miradi hiyo. amesema Meja Jenerali (mstaafu), Jacob Kingu

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Mbadala REA, Mhandisi Advera Mwijage amesema kuwa REA imechangia zaidi ya Shilingi Bilioni 2 katika mradi huo na zaidi ya Shilingi Bilioni 60 kwa miradi ya waendelezaji binafsi kwa Mkoa wa Njombe, huku akiendelea kutoa wito kwa waendelezaji binafsi kushirikiana na REA kuendeleza miradi yao ili kuongeza umeme katika gridi ya Taifa.

“Kazi moja wapo kubwa ya Wakala wa Nishati Vijijini ni kushirikiana na waendelezaji binafsi kwa ajili ya kuhakikisha tunaongeza umeme katika gridi ya Taifa. Lakini umeme huo unaongezwa katika gridi ya Taifa lakini umeme huo unaoongezeka unazalishwa kutoka kwenye vyanzo ambavyo havichafui mazingira ambavyo ni vyanzo vinavyotokana na nishati jadidifu  kama maporomoko ya maji,umeme jua pamoja na upepo,’’amefafanua mhandisi Advera.

Pia mkurugenzi huyo ameendelea  kutoa wito kwa wananchi kutunza mazingira  katika vyanzo vya maji ili kusaidia miradi hiyo ya kuzalisha umeme kwa njia ya maporomoko ya maji kuwa na tija iliyokusudiwa.

Awali akizungumza, Askofu wa Kanisa la KKT Dayosisi ya Kusini Kati Makete, Askofu Wilson Sanga ameishukuru REA kwa kutoa fedha zilizowezesha mradi huo kukamilika.

Ujenzi wa mradi huo unaotekelezwa na Kampuni ya Nishati Lutheran Investment Ltd inayosimamiwa na Kanisa la KKT Dayosisi ya Kusini Kati na ulianza rasmi mwaka 2021 na kumalizika Septemba 2023 ambapo unagharimu zaidi ya Shilingi Bilioni 4.
“Kanisa ni sehemu ya jamii na hivyo linawajibu wa kutatua changamoto zinazoikabili jamii na ndio maana tukaja na wazo la kuanzisha mradi huu ili uweze kuhudumia kituo chetu kinachosaidia watoto  wenye mahitaji maalum cha UDIAKONIA. Na mradi huu haujanufaisha kituo hiki tuu pekee bali hata jamii inayotuzunguka na Kata Zaidi ya Tano zimenufaika na mradi huu wa umeme wa Ijangala,” amesema Askofu Sanga.