Jumatatu , 15th Jul , 2024

Nyota Angel di Maria ametangaza rasmi kustaafu kuitumikia timu ya Argentina baada ya kuitumikia kwa miaka 16 huku akiiongoza miamba hiyo ya Amerika Kusini kushinda taji la Copa America la 16 dhidi ya Colombia leo Alfajiri ya Julai 15-2024 nchini Marekani.

(Nyota wa Argentina Angel di Maria)

Di Maria mwenye umri wa miaka 36 maarufu kwa jina la utani la El Fideo ameitumikia Argentina maarufu kama Albiceleste kwenye michezo 145 na kuifungia magoli 31 ndani ya miaka 16 kuitumikia timu hiyo.

Angel di Maria ameshiriki kwenye fainali  4 za kombe la Dunia (2010,2014,2018 na 2022) huku akishinda kombe la Dunia 2022 nchini Qatar huku alikuwepo kwenye fainali mbili za Copa America 2015 na 2016 wakipoteza mbele ya timu ya  Chile

Ilhali ameshinda taji la Copa America 2021 pamoja na 2024 huku alishinda kombe la Dunia U-20 mnamo 2007 pamoja na kushinda medali ya dhahabu ya michezo ya Olimpiki ya Beijing 2008 nchini China