Jumatatu , 18th Dec , 2017

Winga wa klabu ya Atletico Madrid na timu ya taifa ya Ufaransa Antoine Griezmann ameomba radhi baada watu wengi kuonesha kukerwa na kitendo chake cha kujipaka rangi nyeusi kama sehemu ya utani wa kubadilisha sura.

Griezmann aliweka picha kwenye mtandao wa Twitter ikimwonesha amejipaka rangi nyeusi na kuvaa nywele nyeusi kabla ya mashabiki wake kuanza kumtupia maneno kuwa anachofanya ni ubaguzi wa rangi na sio utani.

Baada ya muda Griezmann aliitoa picha hiyo na kuwaomba mashabiki wake wawe watulivu akieleza kuwa alifanya vile kwa kuwa yeye ni shabiki mkubwa wa timu ya mchezo wa Kikapu Harlem Globetrotters na kupitia hiyo picha alikuwa anatoa heshima kwao.

Hata hivyo baada ya maelezo yote Griezmann amelazimika kuomba msamaha kwa mashabiki wake ambapo kupitia ukurasa wake wa Twitter ameandika, "Natambua kwamba natakiwa kuwa makini, iwapo nimewakera baadhi ya watu, basi naomba radhi."