Jumamosi , 2nd Apr , 2016

Timu za Yanga na Azam fc leo wanaanza kusaka alama tatu muhimu kwa kula viporo vya michezo yao ya ligi kuu baada ya kushinda michezo yao ya robo fainali ya kombe la shirikisho na kutinga nusu fainali ya michuano ya FA Tanzania bara.

Kikosi cha mabingwa watetezi wa ligi kuu ya soka Tanzania bara Yanga ya Dar es Salaam.

Wawakilishi wa Tanzania katika michuano ya vilabu barani Afrika timu za Yanga na Azam jumapili hii wanarejea katika ngarambe za ligi kuu ya soka Tanzania bara VPL kwakucheza michezo yao ya viporo.

Yanga ambao ni mabingwa watetezi wa ligi hiyo wao watakuwa nyumbani katika uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam kuwaalika wanankulukumbi wakata miwa wa Kagera timu ya Kagera Sugar katika mchezo ambao Yanga yenye alama 50 itahitaji ushindi ili iweze kupunguza pengo la alama na Simba wanaoongoza katika msimamo wakiwa na alama 57.

Pamoja na Yanga kupewa nafasi kubwa yakuibuka na ushindi katika mtanange huo lakini pengine hali inaweza kuwa tofauti kwani kutokana na nafasi waliyopo wakatamiwa hao toka Bukoba wakiwa nafasi ya 11 kwa alama zao 25 hivyo ni wazi watataka kupata angalau kama si ushindi basi waambulie angalau alama moja kwa kulazimisha sare.

Wakati hayo yakiendelea kwa Yanga wapinzani wao kwa sasa timu ya Azam fc ambayo nayo in alama 50 katika msimamo wa ligi hiyo kama ilivyo kwa Yanga, wao wamesafiri hadi jijni Mwanza kwenda kuvaana na wagumu wanakishamapanda timu ya Toto Africans katika mchezo ambao kama ilivyo kwa Yanga Azam nao wanahitaji alama tatu muhimu ili kuendelea na mbio za ubingwa wakiifukuza timu ya Simba yenye alama 57, lakinibado suala hilo linakuwa gumu kulibashiriki hasa kutokana na uwezo wa Toto Africans hasa ikiwa katika dimba la nyumbani la CCM Kirumba.

Wakati huo huo klabu ya soka Yanga itakosa huduma muhimu ya kiungo wake mahili, Haruna Hakizimana Niyonzima kesho katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Kagera Sugar utakaopigwa katika uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Nahodha huyo wa Rwanda anasumbuliwa na Malaria, hivyo hatakuwemo kabisa kwenye programu ya mechi mbili zijazo za Yanga.

Baada ya mechi na Kagera Sugar kesho, Yanga watarudi dimbani kwenye Uwanja huo huo Jumamosi ijayo kumenyana na Al Ahly ya Misri katika Ligi ya Mabingwa ya Afrika.

Na Niyonzima hatacheza mechi dhidi ya Ahly kwa sababu atakuwa anatumikia adhabu ya kadi mbili za njano alizopewa kwenye mechi mfululizo za Raundi ya Kwanza ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya APR ya kwao, Rwanda.

Pamoja na kumkosa kiungo wa Amavubi kesho, habari njema ni kwamba Nahodha wa timu, beki Nadir Haroub 'Cannavaro' sasa yuko fiti kabisa kurejea uwanjani.

Cannavaro alicheza kwa dakika tano za mwisho katika mchezo dhidi ya Ndanda FC Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alhamisi Yanga ikishinda 2-1 baada ya kukosekana tangu Novemba mwaka jana alipoumia akiichezea timu ya taifa dhidi ya Algeria mjini Blida.