Jumatatu , 15th Mei , 2017

Kocha msaidizi wa Yanga SC, Juma Mwambusi amefunguka kwa kudai mechi yao ya kesho dhidi ya Toto Africans itakuwa ngumu na yenye ushindani mkubwa kutokana na kile anachokiamini kuwa wapinzani wao wataingia dimbani kwa kuwakamia ili wapate ushindi.

Kocha msaidizi wa Yanga SC, Juma Mwambusi

Mwambusi amebainisha hayo huku akisema benchi lake la ufundi limewaanda vyema wachezaji wake kucheza kwa ushindani ili washinde mechi hiyo na kujiweka katika mazingira mazuri ya kubeba ubingwa wa Ligi kuu.

"Tunatambua Toto kesho watacheza kwa tahadhari kubwa ili kupata ushindi wa alama tatu ili wasishuke daraja na uchovu {fatigue} lakini tumewaandaa vyema wachezaji kimbinu, kiufundi na kisaikolojia ili kushinda uchovu na kucheza kwa moyo wote".Alisema Mwambusi

Aidha, Mwambusi aliendelea kwa kusema anafahamu mipango ya wapinzani wao kuwa wataingia uwanjani kwa kuwakamia ili waweze kujinasua katika kitanzi chao cha kushuka daraja lakini timu yake inalifahamu hilo pamoja na kuwa uzoefu nalo kama ilivyokuwa katika mchezo wao wa jumamosi iliyopita dhidi ya Mbeya City.

 "Tunafahamu watakuja kwa kukamia dhidi yetu na tumejiandaa vyema kiufundi kwa hilo . Kushinda mchezo wa kesho ni muhimu sana kwetu kuelekea ubingwa hivyo tahadhari zote tumechukua”. Alisema Mwambusi

Pamoja na hayo, timu ya Yanga SC watashuka dimbani kuvaana na Toto Africa katika uwanja wa Taifa majira ya saa 10:00 jioni ikiwa ni mechi yao ya 29 kuelekea mwishoni mwa msimu wa ligi kuu na alama zao 65 kileleni mwa ligi.