Jumatano , 13th Dec , 2017

Wawakilishi wa Tanzania katika michuano ya kimataifa ngazi ya klabu msimu wa 2017/18 Simba na Yanga, watajulikana leo ambapo droo ya kupanga hatua ya awali ya michuano hiyo itafanyika jijini Cairo, Misri.

Yanga ambao ni mabingwa wa Tanzania Bara wanasubiri kuwajua wapinzani wao katika michuano ya Klabu Bingwa Afrika na wakati Simba SC wao wakisubiri kujua wataanza na nani katika Kombe la Shirikisho.

Michuano hiyo huandaliwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF). Tayari kamati kuu ya utendaji ya shirikisho hilo imeshaanza vikao vya awali tangu Disemba 11 mwaka huu ikijadili maboresho mbalimbali yanayohitajika kufanyika kwenye michuano hiyo.

MKutano huo unaojulikana kama (CAF interclubs competitions think-tank 2017) unatarajia kutoka na uamzi wa juu ya nini kifanyike ili kuboresha michuano hiyo na hii huenda ikaangukia kwenye kubadili muundo wa mashindano hayo.

Tayari klabu zote za Simba na Yanga zimeshawasilisha majina ya usajili wa wachezaji wao kwa ajili ya michuano ya klabu bingwa na Kombe la Shirikisho Afrika. Mabingwa watetezi wa klabu bingwa ni Wydad Casablanca ya Morocco wakati mabingwa watetezi wa Kombe la Shirikisho ni TP-Mazembe ya DR Congo.