Jumamosi , 16th Dec , 2017

Nyota wa klabu ya soka ya Real Madrid na timu ya taifa ya Ureno Cristiano Ronaldo, amesema anajisikia vyema kutimiza malengo yake kwenye ulimwengu wa soka na anafuraha kushindana na Lionel Messi kwa muda mrefu.

Akifanya mahojiano na tovuti rasmi ya FIFA, Ronaldo amesema ndoto yake ilikuwa kuweka historia na kuacha kumbukumbu kwenye ramani ya soka na hicho kitu kimetimia akiwa ametwaa mataji mengi pamoja na mafanikio binafsi ikiwemo tuzo tano za Ballon d’Or.

“Najisikia vizuri kutimiza malengo yangu, nilitamani sana kuweka historia kuacha jina langu kwenye vitabu vya soka, nimepata mafanikio mengi sana ngazi ya klabu na taifa, nafurahia kuwa mmoja wa wachezaji waliofanikiwa zaidi kama kuchukua tuzo tano sawa na Messi”, amesema Ronaldo.

Ronaldo ameongeza kuwa katika maisha yake amefanya kitu anachokipenda zaidi ambacho ni kucheza soka na amefanikiwa sana na hiyo inamuhamisha kuendelea kufanya vizuri akiwa bado anapenda soka kwasababu utafika wakati hawezi tena kufanya hivyo.

Ronaldo ameshinda taji la Ligi Kuu ya England EPL mara tatu akiwa na Manchester United kabla ya kutua Real Madrid na kushinda ubingwa wa La Liga mara mbili. Pia ameshinda taji la ligi ya mabingwa barani Ulaya UEFA mara nne.