Alhamisi , 16th Jun , 2022

Nyota mpya wa klabu ya Simba Moses Phiri, amefunguka kuwa ndoto yake imetimia baada ya kufanikiwa kutua katika kikosi na kusaini mkataba wa miaka miwili.

Straika wa Simba Moses Phiri

Phiri raia wa Zambia amesema Simba ni timu kubwa katika ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati na alitamani siku moja kucheza hapa ingawa amefuatwa pia na timu nyingine za hapa nchini.

“Ndoto yangu imetimia, nilikuwa natamani kucheza soka la Tanzania. Timu kadhaa zilinifuata lakini nimeichagua Simba. Marafiki zangu (Clatous Chama na Rally Bwalya) waliniambia kuwa hii timu kubwa na menejimenti yake ni nzuri na iko makini,” amesema Phiri.

Phiri ameongeza kuwa anajua Simba ni timu kubwa inashiriki michuano mikubwa inagombania ubingwa wa ligi kila msimu na mashabiki wanahitaji furaha lakini hana presha kwa kuwa soka ni kazi yake.

Kuhusu michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao ambao malengo yetu ni kufika nusu fainali, Phiri amesema kwa kushirikiana na wachezaji wenzake na benchi la ufundi anaamini tutafikia matarajio yetu.