Jumapili , 30th Mar , 2025

Kylian Mbappe ameifikia rekodi ya Cristiano Ronaldo ya kufunga magoli 33 katika msimu wake wa kwanza akiwa Real Madrid baada ya kufunga magoli mawili katika ushindi wa 3-2 wa timu yake dhidi ya Leganes hapo jana katika Uwanja wa Bernabeu.

Cristiano Ronaldo na Kylian Mbappe

Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ufaransa alifunga goli la kwanza kwa mkwaju wa penalti, kabla ya kufunga goli lake la pili kwa mkwaju wa faulo katika dakika ya 76 na kuipa Real Madrid alama tatu muhimu zinazowabakiza katika mbio za ubingwa wa La Liga Msimu huu.

Mbappe sasa amefikisha mabao 33 katika mechi 45 alizocheza Real Madrid msimu huu, akilingana na jumla ya mabao ya Cristiano Ronaldo katika msimu wake wa kwanza katika klabu hiyo msimu wa 2009-10, ingawa Mreno huyo alicheza michezo 35 pekee msimu huo.

Akizungumzia kusawazisha jumla ya mabao 33 ya Ronaldo katika kampeni yake ya kwanza, Mbappe alisema: "Ni maalum sana, Mambo muhimu zaidi ni mambo unayofanya ukiwa na timu, lakini kuwa na idadi ya mabao sawa na Cristiano siku zote ni nzuri.

"Tunajua anachowakilisha Real Madrid na kwangu, Tunazungumza kila mara na ananipa ushauri mwingi. Lakini kama ninavyosema siku zote, lazima tushinde mataji."