Jumatano , 29th Jun , 2016

Mshambuliaji Manuel Agudo Durán Nolito anayekipiga na klabu ya Celta Vigo ya Hispania anatarajiwa kufanyiwa vipimo vya afya muda wowote kuanzia sasa tayari kwa kukamilisha uhamisho wake wa kutua ndani ya klabu ya Manchester City.

Manuel Nolito (pichani)akifanya yake akiwa na Celta Vigo katika La Liga

Nolito mwenye umri wa miaka 29 alinukuliwa akikana kufanya mazungumzo na klabu yoyote hivi karibuni wakati akihusishwa kwake kutaka kuhamia katika klabu za Barcelona na Manchester City ya England.

Ripoti za vyombo vya habari mbalimbali nchini Uingereza zimearifu kuwa nyota huyo atasafiri kuelekea nchini humo leo kwa ajili ya kukamilisha usajili huo unaotajwa kuigharimu Manchester City kiasi cha pauni milioni 13.8.

Rekodi zinaonesha kuwa nyota huyo alifunga mabao 12 katika michezo 29 msimu uliopita na atakuwa mchezaji wa pili kusajiliwa na kocha Pep Guardiola ndani ya Manchester City baada ya Ilkay Gundogan.