Jumatatu , 18th Dec , 2017

Makamu wa Rais wa pili wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameipongeza timu ya taifa ya Zanzibar (Zanzibar Heroes) ambayo imeshika nafasi ya pili kwenye michuano ya CECAFA 2017.

Balozi Seif Iddi ametoa pongezi hizo leo mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli wakati akiwasilisha ripoti ya utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwenye mkutano mkuu wa chama mjini Dodoma.

“Mh. Rais na wajumbe wote wa mkutano huu mkuu wa tisa naomba kwa nafasi ya pekee niwapongeze vijana wa Zanzibar Heroes ambao wamelitoa taifa kimasomaso baada ya kushika nafasi ya pili kwenye CECAFA huko Kenya”, amesema Balozi Seif.

Zanzibar Heroes imewasili mjini Unguja leo asubuhi kwa ndege na kupokelewa na mamia ya mashabiki. Timu hiyo imepata nafasi hiyo baada ya kufungwa na Kenya kwa mikwaju ya Penalti 3-1 kwenye fainali iliyopigwa uwanja wa Kenyata Machakos Kenya.