Ijumaa , 20th Jun , 2014

Baadhi ya wanachama wameonesha kukerwa na maamuzi ya kamati ya rufani ya uchaguzi ya TFF kwa kuikataa rufaa ya Wambura Michael huku baadhi yao wakisema haki imetendeka na wakimtaka mgombea huyo kuheshimu maamuzi ili kuleta amani klabuni hapo

Aliyekua mgombea urais wa klabu ya Simba Michael Wambura wakati huo akirudhisha fomu za kuwania nafasi hiyo.

Siku moja baada ya kamati ya rufani ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kuikataa rufani ya Michael Wambura kupinga kuenguliwa kugombea urais wa klabu ya Simba unaotarajiwa kufanyika baadaye mwezi huu

Hii leo baadhi ya wanachama wa klabu hiyo wametoa maoni yao tofauti juu ya uamuzi huo wa kamati ya rufani ya TFF
Ambapo Kasey Joseph yeye amepinga uamuzi huo nakusema watakwenda TFF kulalamikia maamuzi hayo huku mwenzie Mgeni Ramadhani ‘dogo macho’ akiunga mkono uamuzi huo na kuwataka wanasimba kuwa watulivu na kujipanga kuchagua kiongozi ambaye ataivusha klabu ya Simba toka hapa ilipo na kuirejesha katika makali yake ambayo kwa misimu kadhaa sasa timu hiyo imeonekana kupoteza mwelekeo

Aidha Mgeni 'dogo macho' ameongeza kusema ni wakati sasa kwa mgombea huyo [Wambura] kuheshimu maamuzi ya kamati hiyo kwani ni kamati makini inayoundwa na wasomi na waliobobea katika sheria, hivyo ni wakati sasa kwa yeye kutumia busara na kuinusuru Simba hasa katika kipindi hiki ambacho mambo mengi ya klabu hiyo yamesimama likiwemo zoezi la usajili ili kupisha zoezi la uchaguzi mkuu wa klabu hiyo ambao mpaka sasa majaliwa yake yako mikononi mwa wagombea na wanachama wenyewe wa klabu hiyo.