Alhamisi , 11th Oct , 2018

Kaimu Mkurugenzi wa idara ya maendeleo ya watoto Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mwajuma Magwiza, amewataka walimu nchini kutowabagua watoto kutokana na uwezo wao darasani.

Picha haina uhalisia na kilichosemwa, imetumika kama mfano.

Mwagwiza ameyasema hayo leo kwenye MJADALA wa East Africa Television, ikiwa ni siku ya mtoto wa kike duniani, ambapo amebainisha kuwa walimu wanapaswa kutenda haki darasani bila kuwabagua watoto kwa uwezo wao ama jinsia zao.

''Watoto wote wapewe nafasi bila kubaguliwa tunajua wanatofautiana uwezo lakini hiyo haifanyi wengine watengwe na sidhani kama hiyo ni maadili ya ualimu labda ni tabia binafsi za mtu'', amesema Magwiza.

Hatua hiyo imekuja baada ya mtoto Rahabu Francis ambaye naye alikuwepo kwenye MJADALA, kueleza kuwa amewahi kukumbana na kadhia hiyo ya kushuhudia wenzake wakitengwa darasani kisa uwezo, kupitia walimu kuunda klabu za kujisomea na ambazo hazizingatii uwezo wanafunzi.

Aidha Magwiza amewataka wazazi nao kutimiza wajibu wao kwa kuhakikisha wanafuatilia mienendo ya watoto wao wa kike na kuwatimizia mahitaji yao ili kuwaepusha na vishawishi ambavyo mwisho wa siku vinapelekea madhara kama mimba za utotoni.