Ijumaa , 16th Feb , 2018

Mchekeshaji maarufu nchini Tanzania, Mzee Majuto amefunguka na kuweka wazi kwamba sinema ndio kitu pekee kinachomfanya aweze kutamba mjini 'kuishi' huku akidai ana kazi nane ameshazifanya ameziweka ndani tu, na uganga basi ndio imetoka.

Mzee Majuto amesema hayo wakati alipokuwa akipiga stori mbili tatu alipotembelewa na wasanii wenzake Jacob Stephen 'JB' pamoja na Single Mtambalike 'Richie', katika hospitali ya Tumaini Jijini Dar es Salaam alipolazwa kwa ajili ya kupatiwa matibabu yake.

"Nina miaka 70 mpaka hivi sasa na ninaishi kutokana na sinema, nina 'movie' nane nimeziweka ndani sina presha. Nikisikia njaa natoa moja nauza napata kula. Katika hizo nane nimeuza moja tu inaitwa uganga basi", amesema Mzee Majuto  

Mwishoni mwa mwezi Januari mwaka huu Mzee Majuto alipelekwa katika hospitali ya Tumaini iliyopo Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kufanyiwa matibabu ya ugonjwa wa tezi dume ambao ulianza kumsumbua takribani miezi miwili iliyopita toka sasa.