Jumamosi , 17th Aug , 2024

Kutokana na taarifa za Shirika la Afya Duniani (WHO), kuhusu ugonjwa wa Mpox zinaeleza kuwa hadi June 2024, jumla ya wagonjwa 99,176 na vifo 208(0.2%) vimethibitishwa duniani kote, huku taarifa zikionyesha kuwepo kwa mlipuko wa ugonjwa huu katika baadhi ya mataifa jirani na Tanzania.

Ugonjwa wa M pox

Hali hiyo imepelekea kuhitajika hatua za tahadhari kwa kila Mtanzania kuhakikisha ugonjwa huu hauingii nchini.

Kupitia taarifa iliyotolewa na Wizara ya Afya nchini imeeleza kuwa  wameendelea kuchukua hatua mbalimbali kuzuia kuingia nchini ugonjwa wa Mpox na kuimarisha utayari wa kukabiliana nao ikiwa pamoja na kuandaa na kusambaza vipeperushi vya elimu ya jamii kuhusu dalili na njia za kujikinga na ugonjwa wa Mpox. 

Vilevile, wizara imeimarisha mifumo ya ufuatiliaji wa ugonjwa huu katika ngazi zote; kuandaa miongozo ya tiba na kinga kwa watumishi; pamoja na kuimarisha uwezo wa maabara ya Taifa ya Afya ya Jamii ili kuweza kupima sampuli za wahisiwa wa ugonjwa wa Mpox.

Ndugu wananchi, Mpaka sasa, hakuna mgonjwa yeyote aliyethibitika kuwa na maambukizi ya Mpox na nchi yetu ni salama. 

Hata hivyo, tunahitaji kuendelea kuchukua tahadhari kujikinga na ugonjwa huu.