Alhamisi , 14th Jan , 2016

Zaidi ya Wafugaji 200 kutoka kijiji cha Wami Dakawa kilichopo wilaya Mvomero mkoani Morogoro wameandamana wakiulalamikia uongozi wa Kijiji hicho kuuza eneo lenye ukubwa wa hekari zaidi ya 600 bila kushirikishwa.

Wanakijiji wa Wami Dakawa wakiongozana kupinga uuzwaji wa ekari zaidi ya 600

Wakizungumza kwa uchungu wakazi hao wamesema kuwa mpaka sasa hali imesababisha kukosa mashamba ya kulima pamoja na sehemu za malisho hali inayowafanya kutishia uvunjifu wa amani kati yao na mwekezaji huyo.

Wakazi hao wamesema imefikia wakati wanatishia usalama wao na walinzi wa eneo hilo kwa silaha za moto huku wengine wakisema kuwa kutokana na muwekezaji huyo kuweka uzio eneo hilo wanakosa njia ya kwenda mashambani mwao kutafatua chakula hali inayoweza kuwasabishia baa la njaa.

Akitolea Majibu ya lawama hizo za wanakijiji hao mwenyekiti wa Kijiji hicho cha Wami Dakawa Bw. Abdallah Mgaya amesema kuwa eneo hilo linamilikiwa na muwekezaji huyo kihalali na kuwataka wanakijiji hao kuacha kuvamia maeneo ambayo sio yao ili kuondoa migogoro isiyo ya lazima.