Ijumaa , 28th Aug , 2020

Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Idara ya Uhamiaji, imewataka wageni wanaoingia nchini kwa shughuli za utalii, biashara ama kazi kuhakikisha wamefuata taratibu za kupata vibali halali.

Aidha Idara hiyo imewataka wananchi kuwa makini pamoja na kutoka taarifa endapo wataona  uwepo wa raia wa kigeni ambao wameingizwa kinyemela hasa katika kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu Oktoba 28.

Rai hiyo imetolewa hii leo na Msemaji wa Idara ya Uhamiaji Mrakibu Paul Mselle ambaye amesema kama idara wamekuwa wakishirikiana na Tume ya Taifa ya uchaguzi katika kutoa Elimu ya Uraia na Mpiga Kura ili kumsaidia mwananchi kufanya maamuzi sahihi kuchagua kiongozi anaemtaka.

Aidha amesema kwa nchi nzima kuna zaidi ya vituo 60 ambavyo mgeni anaweza kuingia akapata huduma ya kupewa kibali cha kuingia nchini kwa njia halali kwa kada zote iwe kibiashara, kikazi ama kufanya utalii huku akiweka wazi kwa sasa hali ya wageni kuja nchini ipo kwa kiasi gani mara baada ya janga la Covid-19.

Idara ya Uhamiaji imewaasa watu wasio Watanzania kutojihusisha na uchaguzi kwa kuwa ni kinyume na sheria za nchi.