Alhamisi , 13th Mar , 2025

Msafara wa Viongozi wa ACT Wazalendo ukiongozwa na Kiongozi wa chama hicho Dorothy Semu na Mwenyekiti wa chama Othman Masoud Othman, ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar umezuiwa kuingia nchini Angola na mamlaka za serikali za nchi hiyo.

Wengine waliozuiliwa na Mamlaka za uhamiaji nchini Angola ni Mwenyekiti wa CHADEMA Tundu Lissu pamoja na ujumbe wa viongozi zaidi ya 20 ambao ni wawakilishi wa vyama vya siasa kutoka Kusini mwa Afrika

Viongozi hao wanashikiliwa katika uwanja wa ndege wa Luanda na hati zao za kusafiria zinashikiliwa na serikali ya Angola, bila kueleza sababu yoyote imetoa amri ya viongozi hao kurejeshwa Tanzania hii ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolea na ACT Wazalendo

"Viongozi hao waliwasili Angola kushiriki mazungumzo ya Jukwaa la Demokrasia Afrika yaliyoandaliwa na Taasisi ya The Brenthurst Foundation yaliyopangwa kufanyika kuanzia tarehe 13-16 Machi 2025," imeeleza taarifa hiyo

Mbali na viongozi wa ACT Wazalendo, viongozi wengine zaidi ya 40 kutoka nchi mbalimbali Afrika ambao pia walikuwa wanahudhuria mkutano huo wamezuiliwa na serikali ya Angola. Moja ya viongozi waandamizi waliotarajiwa kushiriki kwenye Mkutano huo ni pamoja na Marais Wastaafu Ian Khama (Botswana) na Andres Pastrana Arango (Columbia).

Wengine ni Waziri wa Kilimo wa Afrika ya Kusini na kiongozi wa Chama cha DA John Steenhuisen na Kiongozi wa chama cha PODEMOS cha nchini Msumbiji Venancio Mondlane.