Jumamosi , 14th Sep , 2024

Viongozi wa soko la wazi la Machinga lililopo Mtaa wa Kitenge, Kata ya Majengo katika Jiji la Dodoma, wamesimamishwa uongozi kupisha uchunguzi kutokana na kudaiwa kutenda makosa ya kiuongozi na kijinai kwa wafanyabiashara wa soko hilo.

Agizo hilo limetolewa Septemba 13, 2024 na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule alipokua akitatua kero za wafanyabiashara wa soko hilo katika Mkutano wa hadhara aliouitisha ndani ya soko hilo.

Wafanyabiashara hao, walipata fursa ya kutoa kero zao mbele ya Kiongozi huyo lakini kubwa zaidi ni lawama walizotupiwa viongozi wa soko ambao ni Mwenyekiti na Meneja kwa kuuza vizumba kinyume na taratibu pia kughushi barua za Mkurungenzi wa Jiji pamoja na vitambulisho vya wajasiriamali.

"Zipo tuhuma za kiuongozi lakini nyingine za jinai kama kufoji vitambulisho na barua. Hatuna uhakika mpaka uchunguzi ufanyike. Wakati uchunguzi unafanyika Mwenyekiti na Meneja wasimamishwe kwani wameonekana katika sehemu kubwa ni sehemu ya tatizo." Ameagiza Mhe. Senyamule.

Hata hivyo, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini Mhe. Jabir Shekimweri, alisema awali aliunda timu ya uchunguzi ikiongozwa na Kamishna wa TAKUKURU Wilaya kutokana na kero za wafanyabiashara hao alipowasikiliza awali na ilikua na mapendekezo kadhaa ikiwemo kwenye ulipaji ushuru wa siku.

"Kwenye suala la ulipaji ushuru wa soko, Tume ilipendekeza wafanyabiashara wote wasajiliwe kwenye Mfumo na kulipa mara moja au mbili kwa mwezi lakini wapewe control number ya malipo ili yaende moja kwa moja kwenye mfuko wa Serikali na sio mfukoni kwa mtu". Amesema Mhe. Shekimweri.

Naye Mkurungenzi wa Jiji la Dodoma Dkt. Fredrick Sagamwiko, amesema ofisi yake ipo mbioni kukamilisha Mfumo mpya wa uendeshaji wa soko ambao unatarajiwa kuanza mapema mwezi Oktoba ambao utakwenda kutatua kero zote za wafanyabiashara hao na kuanzia Septemba 17, 2024, wataanza uhakiki wa kupata idadi kamili ya wafanyabiashara wenye vizimba katika soko hilo.

Soko la Machinga Jijini Dodoma, lilianza kujengwa mwaka 2022 kufuatia agizo la Rais wa Tanzania kutaka wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu kama Machinga wapatiwe eneo maalum la biashara ili kuweka safi Mazingira ya Jiji na limegharimu takribani shilingi Bilioni 9 fedha kutoka Serikali kuu pamoja na mapato ya ndani ya Jiji na linabeba wafanyabiashara zaidi ya 3,000