Jumapili , 13th Mar , 2016

Mfumo wa elimu nchini Tanzania hauwaandai vijana kuwa na hali nzuri ya kiuchumi na kwamba kuna hatari vijana wengi nchini watakapofikisha umri mkubwa uzeeni uzee wao hautakuwa wa staha.

Miradi wa Help Age nchini Tanzania Bw. Joseph Mmbasha.

Kauli hiyo imetolewa jijini Dar es Salaam leo na Shirika linalojihusisha na ufuatiliaji wa haki na maslahi ya wazee lenye makao yake makuu nchini Uingereza la Help Age International ambalo lina ofisi na kuendesha shughuli zake nchini.

Meneja Miradi wa Help Age nchini Tanzania Bw. Joseph Mbasha amesema hayo katika mahojiano na EATV jijini Dar es Salaam na kufafanua kuwa hali ni mbaya zaidi kwani hata wale wachache wenye bahati ya kuwa na kipato hawana tabia ya kutunza akiba ya hicho walichonacho ili kiwatunze uzeeni.

Mbasha amesema kuna haja ya serikali kuanda mitaala itakayotoa mafunzo na malezi bora ya watoto ili wanapofika umri wa ujana watambue kuwa siku moja na wao watakuwa wazee na hivyo wajijengee utamaduni wa kuweka akiba sambamba na kufanya kazi kwa bidii ili kuwa na kipato kitakachowasaidia wanapofikisha umri wa uzee.

Kwa mujibu wa Mbasha, vijana ndiyo wazee watarajiwa na kwamba kuna hatari ya taifa kuwa na kundi kubwa la wazee wenye maisha yasiyo na staha iwapo hakuna juhudi za makusudi za kuwaandaa vijana kuwa na nguvu ya kiuchumi huku wakijiwekea akiba ya kipato kidogo wanachokipata wakati wa ujana.

Mbasha amesema mkazo unaweza kuwekwa kwenye hifadhi ya jamii ili kuwa na mfumo utakaoangalia ni kwa namna gani vijana nchini wanajiunga na hifadhi ya jamii ili kuwe na utaratibu unaoeleweka wa kuwahudumia wanapofikia uzeeni.