Jumatatu , 11th Dec , 2017

Rais wa Venezuela Nicolas Maduro amesema vyama vikubwa vya upinzani nchiNi humo vimezuiwa kushiriki kwenye uchaguzi ujao wa urais ambao unatarajiwa kufanyika mwaka 2018.

Rais Maduro amesema vyama pekee ambavyo vitashiriki ni vile ambavyo vimeshiriki kwenye uchaguzi wa meya uliofanyika Jumapili iliyopita, ambao vyama hivyo vikubwa vilisusia.

Kufuatia tukio hilo Rais Maduro amesisitiza kwamba mfumo wote wa uchaguzi wa nchini humo ni wa kuaminika, na kwamba vyama hivyo vimejipoteza kwenye ramani ya siasa.

“Chama ambacho hakijashiriki kwenye uchaguzi huu hakitashiriki tena, kwani wamejiondoa kwenye ramani ya siasa”, amesema Rais Maduro.

Viongozi wa vyama vya Justice First, Popular Will na Democratic Action walisusia uchaguzi wa meya, wakisema kwamba mfumo wa upigaji kura sio wa haki.

Mwezi Oktoba mwaka huu vyama vitatu vikubwa vya siasa nchini Venezuela vilitangaza vitasusia uchaguzi wa meya, ambao umefanyika Jumapili hii kwenye miji 300 ya nchi hiyo, wakisema uchaguzi huo unampendelea Rais aliyeko madarakani Nicolas Maduro.