Jumamosi , 7th Jul , 2018

Mbunge wa Iramba Magharibi, Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka wakazi wa jimbo hilo kutosikiliza maneno ya watu wanaosema kuwa anaweza jiuzulu nafasi ya ubunge baada ya kuondolewa katika baraza la Mawaziri.

Mbunge wa Iramba Magharibi, Dkt. Mwigulu Nchemba akiwa jimbo kwake.

Dkt. Mwigulu alitoa kauli wakati akiwa kwenye mkutano na wakazi Kata ya Ulemo kijiji cha Misigiri wilayani Iramba mkoani Singida.

"Uongozi ni kupokezana kijiti na si kwamba kweli nina lengo la kuacha nafasi yangu ya Ubunge. Nitaendelea kuwatumikia wananchi wa jimbo langu kwa muda wote tofauti na awali nilivyokuwa kwenye majukumu ya kitaifa. Hao wanaosema nataka kujiuzulu Ubunge, wanataka kutengeneza jambo la ugomvi, lakini kwangu sioni kama ni ugomvi wala tatizo nimerudi kuwa tumikia wananchi wa jimbo kwa kazi mlionituma", amesema Mwigulu.

Kwa upande mwingine, Mwigulu ametumia nafasi hiyo kumshukuru Rais John Magufuli kwa kumwamini na kumpa na nafasi katika serikali yake hadi alipombadilisha na hana kinyongo chochote, ataendelea kufanya kazi chini ya Mwenyekiti wa CCM na serikali pale itakapoitajika huduma yake.