Jumatatu , 18th Dec , 2017

Katibu Mkuu wa zamani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Yusuf Makamba amesema sifa za pekee ziwaendee waasisi wa Taifa, Julius Nyerere na Abeid Amani Karume kwa kulitetea taifa hadi kufika leo.

Makamba amepata nafasi ya kuongea hayo kwenye mkutano mkuu wa tisa wa Chama cha Mapinduzi mara baada ya Mwenyekiti wa muda Benjamin William Mkapa kumpa nafasi ya kuwasalimia wajumbe na wageni waliohudhuria mkutano huo.

''Tunajipongeza sisi tunasahau waliotengeneza nchi, waasisi Julius Nyerere na Abeid Karume,'' amesema. Akiongea kuhusu utendaji kazi wa Rais Magufuli amesema kwamba anampongeza kwa kufanya mambo kwa kutoogopa  kitu chochote na anafanya kazi kwa weledi.

"Siku moja nilitabiri kuwa Kikwete ana batiza kwa maji, lakini JPM anabatiza kwa moto na sasa yanatimia kupitia matokeo mazuri ya viti vya Udiwani katika uchaguzi mdogo ambayo ni matokeo ya utendaji kazi mzuri wa serikali ya awamu ya tano chini ya CCM”, ameongeza.

Katika hotuba yake ambayo imechukua dakika 13 amewatahadharisha wapinzani kuwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 haitokuwa rahisi kwao kwani Chama Cha Mapinduzi kimejipanga vizuri kuweza kushinda tena.