Jumamosi , 14th Nov , 2015

Ufaransa imetangaza hali ya hatari ikiwa ni pamoja na kufunga mipaka ya nchi hiyo kufuatia mashambulizi ya kigaidi nchini humo yaliyosababisha vifo vya watu zaidi ya 120 mpaka sasa katika shambulio la bomu na bunduki jijini Paris.

Watu 80 inasemekana waliuawa baada ya watu wenye silaha kuvamia tamasha huko Bataclan na kuwateka watu kadhaa, wakati watu wengine waliuawa katika mashambulizi mengine yaliyofanyika katika migahawa maeneo matano tofauti.

Polisi imesema washambuliaji wanane waliuawa ingawa haikufahamika mara moja kama kuna washambuliaji waliofanikiwa kutoroka.

Wakazi wa jiji la Paris wametakiwa kutotoka nje ya nyumba zao huku wanajeshi 1500 wakilitanda jiji hilo kuimarisha ulinzi.

Akiongea baada ya kufika katika ukumbi huo baadaye, Rais wa Ufaransa Francois Hollande ameapa kuwa wahusika watashughulikiwa "bila huruma".

Naye Rais wa Marekani Barack Obama amelitaja shambulio hilo kuwa "jaribio lisilokubalika la kuhangaisha raia wasio na hatia" na kuahidi kusaidia Ufaransa kukabiliana na waliohusika.