Ijumaa , 9th Feb , 2024

Serikali ya Tanzani kupitia kwa Waziri wa Mambo ya Nje ya Nchi na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Januari Makamba amesema Tanzania kama nchi haiko vitani na kundi lolote lile lenye silaha nchini DRC.

Kupitia ukurasa wa mtandao wa X Mhe. Makamba amesema Tanzania ipo DRC kama sehemu ya ujumbe wa SADC (SAMIDRC) ambapo uwepo huo ni matokeo ya uamuzi wa Mkutano wa Wakuu wa SADC uliofanyika Agosti mwaka jana.

“Tuko DRC kama sehemu ya Ujumbe wa SADC (SAMIDRC), ambao ni matokeo ya uamuzi wa Mkutano wa Wakuu wa SADC wa Agosti 2023 wa kukubali ombi la serikali ya DRC, kwa kuzingatia Mkataba wa Ulinzi wa Pamoja wa SADC, kupeleka ujumbe wa kijeshi kuisaidia. kushughulikia changamoto za usalama kwa upande wake wa Mashariki” ameandika Januari Makamba kupitia ukurasa wake wa X

“Tanzania haiko vitani na kundi lolote lenye silaha nchini DRC.” Aliongeza January Makamba,Waziri wa Mambo ya nje Tanzania.

Amesema  nchi za SADC zinachangia wanajeshi na fedha kwa ajili ya Ujumbe huo ambao upo DRC.

Katika ujumbe wake Makamba amewataka wanahabari ambao wamekuwa wakiandika habari kuhusu vikosi vilivyopo DRC kutafuta taarifa sahihi kutoka kwa wahusika kma Sekretarieti ya SADC ama wasemaji wa misheni husika

Tanzania inajifungamanisha na michakato ya Luanda na Nairobi, taratibu za kisiasa za kikanda za utatuzi wa amani wa mzozo wa Mashariki mwa DRC.