Alhamisi , 18th Jul , 2024

Rais Samia Suluhu Hassan amesisitiza wananchi kulipa kodi kwa wakati ili kusaidia utekelezaji wa miradi na kuwatoa shaka wananchi kwamba kinachokusanywa kwenye kodi huwa hakiendi mifukoni mwa viongozi.

Rais Samia Suluhu Hassan

Samia ameyasema hayo leo Julai 18, 2024 aliposimama kusalimiana na wakazi wa eneo la Momba Wilaya ya Tunduma mkoani Songwe ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya kikazi kwenye mikoa mbalimbali nchini.

"Ndugu zangu mazuri yote yaliyotajwa na mema mengine yote yaliyodaiwa serikali ifanye tunafanya kutokana na fedha za kodi na tozo, nakubali wakati mwingine wale tuliowaamini wakusanye kodi wanafanya makosa hilo nalo tunaliangalia tunarekebisha, niwaombe sana kila mmoja katika biashara yake alipe kile anachopaswa kulipa," amesema Rais Samia

Aidha Rais Samia ameongeza kuwa, "Tunachokikusanya hakiendi mifuko kwetu haya yote mamiradi mnayoyasikia ni pesa tunayoikusanya kwa njia ya kodi na tozo, na wakati mwingine haitoshi tunaenda kukopa tunakopa kwenye mashirika ya kimataifa na tunatozwa riba ili kuepukana na hilo lazima tukusanye pesa yetu ndani,".