
MKUU wa Wilaya ya Arumeru, Wilson Nkambaku amezuia viongozi wa serikali za mitaa wanatoa vibali kwaajili ya ujenzi, kwenye vyanzo vya maji, kuacha mara moja kutoa vibali hivyo ili kudhibiti uharibifu wa mazingira.
Bw Nkambaku amesema hayo hii leo Jijini Arusha wakati wa maadhimisho ya siku ya mazingira Duniani yaliyofanyika Kimkoa Halmashauri ya Arusha Vijijini, kwa kupanda miti eneo la chanzo cha Maji cha Kiranyi na baadaye Shule ya Msingi Kiranyi.
Aidha amesema kuwa wale wote waliojenga kwenye maeneo ya vyanzo vya maji Mkoani Arusha nyumba za zitabomolewa, hivyo vema wakahama wenyewe kabla ya kubomolewa ili kulinda vyanzo vya maji huku akiwataka viongozi wa serikali za mitaa kuacha tabia ya kuruhusu maeneo ya vyanzo vya maji pamoja na ujenzi holela unaofanywa na baadhi ya wananchi ikiwemo kuosha magari karibu na mita 60 ya vyanzo vya maji.
Naye Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Richard Kwitega akitoa hali halisi ya uharibifu wa mazingira amesema uelewa mdogo wa sheria ya mazingira ya mwaka2014 ndio chanzo kikubwa cha wanachi kuharibu vyanzo vya maji hali inayochangia kuleta mabadiliko ya tabia nchi.
Maadhimisho hayo yameshirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo ikiwemo wanafunzi wa Shule ya Msingi Kiranyi pamoja na wananchi, ambapo zaidi ya miti milioni 1.5 imepandwa na miongoni mwa miti hiyo ni ya matunda iliyopandwa kwenye shule sita za Mkoa wa Arusha.
