Alhamisi , 30th Jul , 2015

Mbunge wa Kongwa aliyemaliza muda wake ambaye pia ni Naibu Spika wa Bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai amehojiwa na jeshi la Polisi Mkoani Dodoma kwa tuhuma za kumshambulia kwa fimbo na kumjeruhi mgombea mwenzake

Mbunge wa Kongwa aliyemaliza muda wake ambaye pia ni Naibu Spika wa Bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai.

Akithibitisha kuhojiwa kwa Mh. Ndugai, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma amesema kuwa walilazimka kumhoji Mh. Ndugai baada ya kupokea malalamiko kuhusiana na tukio hilo lilitokea wilayani kongwa hivi karibuni lakini baadae walimuacha kwa dhamana na uchunguzi unaendelea.

Tukio hilo limetokea jana jioni wakati wagombea wa ubunge kwa tiketi ya CCM wakiwa kwenye mkutano na wanachama wa CCM kwa ajili ya kujinadi kwenye kata ya Ugogoni iliyopo Wilayani Kongwa Mkoani Dodoma.

Kwa mujibu wa shuhuda wa tukio hilo ambaye pia ni mdogo wa Dk, Chilongani, Michael Chilongani, Ndugai alichukua uamuzi huo baada ya mmoja wa wagombea anayeitwa Simon Ngatunga kusema kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa kuwa na ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma na kuahidi kuwa kama atakuwa mbunge atahakikisha kuwa anaziba mianya yote ya ubadhirifu kauli iliyomkera Job Ndugai.
Ilipofika zamu ya Ndugai kujinadi kwa wanachama wa CCM alimtuhumu Ngatunga kwa kusema uongo na kwamba hakuna ubadhirifu wa aina yoyote ndani ya Halmashauri hiyo.

Amesema Ndugai aliposhuka jukwaani alianza kumtafuta Ngatunga ili ampige kwa fimbo ambayo huwa anatembea nayo kwenye kampeni hizo.

Wakati akifanya fujo za kumpiga mgombea huyo, Dk, Chilongani alikuwa anampiga picha kwa kutumia simu yake ya mkononi ambapo Ndugai alipomwona alianza kumshambulia kwa fimbo katika maeneo ya tumboni na kichwani hali iliyomfanya mgombea huyo kupoteza fahamu papo hapo.