Jumatatu , 18th Dec , 2017

Mbunge wa Arumeru Mashariki Joshua Nassari ameshangazwa na Taasisi ya Kuzuia  na Kupambana na Rushwa kushindwa kuona uhalisia au uongo kwenye ushahidi waliouwasilisha dhidi ya aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Alexander Mnyeti na badala yake,

wameona siasa.

Nassari amesema hayo ikiwa ni siku moja kupita baada ya TAKUKURU kutupilia mbali ushahidi wao kwa kudai kwamba uliharibiwa kwa kuingiza siasa.

Nassari amesema kwamba “Niliwapa takukuru kila aina ya ushahidi walioutaka. Cha ajabu hawajaona uhalisia au uongo uliopo kwenye ushahidi, badala yake wameona siasa. ni kweli ilikuwa lazima waone siasa kwa sababu hata ununuzi wenyewe ulikuwa ni rushwa ya ki-mfumo (systemic corruption ). Na aina hii ya rushwa ni mbaya sana kama itaachwa ikasambaa kwenye mfumo mzima wa Siasa za nchi," Nassari.

Nassari amefafanua kwamba katika kuwasilisha ushahidi wa kununuliwa kwa madiwani aliwakabidhi moja ya kifaa alichotumia kurekodia baadhi ya matukio.

"Niliwapa takukuru mpaka moja ya kifaa nilichotumia kurekodi baadhi ya vikao vya ununuzi na ushawishi wa rushwa. Na wakasema wana teknolojia ya hali ya juu ku-retrieve kazi zote, muda na wakati ambapo video hizo zilichukuliwa, bila kukosea. Teknolojia ambayo mimi pia ninayo".  Ameongeza Nassari