Jumatano , 24th Dec , 2014

Mvua kubwa iliyonyesha jijini Mwanza na kudumu kwa zaidi ya saa moja leo mchana imesababisha mafuriko makubwa katika mtaa maarufu wa maduka ya nguo na bidhaa mbalimbali wa makoroboi.

Hali hiyo imesababisa kusimama kwa pilikapilika za maandalizi ya sikukuu ya krismas zilizokuwa zikiendelea kwa kasi.

Mvua hiyo iliyoanza kunyesha majira ya saa 6.45 mchana na kumalizika saa 8, imesababisha usumbufu mkubwa kwa maelfu ya wakazi wa jiji la Mwanza ambao walikuwa wakifanya manunuzi ya nguo na vyakula kwa ajili ya sikukuu ya Krismasi.

Usumbufu huo umekuja baada ya maduka yote pamoja na njia za waenda kwa miguu katika mtaa huo wa makoroboi kujaa maji, hali ambayo imetibua furaha ya wakazi wa jiji la Mwanza wanaojiandaa kusherehekea sikukuu ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo mfalme zaidi ya miaka 2000 iliyopita huko bethlehemu.

kabla ya mvua hiyo kunyesha, EATV ilipita katika mitaa mbalimbali ya jiji hili na kukuta baadhi ya wananchi wakiendelea na manunuzi ya nguo, vyakula na mapambo.