Jumapili , 18th Feb , 2018

Msimamizi wa uchaguzi mdogo wa Ubunge katika jimbo la Kinondoni ambaye ni Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Aron Kagurumjuli amemtangaza Maulid Mtulia kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa mshindi wa nafasi hiyo.

Kwa mjibu wa Kagurumjuli wakati anatangaza matokeo amesema Maulid Mtulia (CCM) amepata jumla ya kura 30,247 akimshinda mpinzani wake wa karibu Salum Mwalimu (CHADEMA) aliyepata kura 12,355.

Uchaguzi huo ulifanyika jana Februari 17 kwa zoezi la kupiga kura ambalo lilimalizika jioni na shughuli ya kuhesabu kura kuanza ambapo baada ya kukamilika asubuhi hii msimamizi ametangaza matokeo.

Aidha uchaguzi huo umefanyika kufuatia aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo Maulid Mtulia aliyechaguliwa 2015 kupitia chama cha Wananchi CUF kwa mwamvuli wa UKAWA kujiuzulu nafasi hiyo na kuhamia CCM.

Mtulia ameungana na Godwin Mollel kuwa wabunge wapya ndani ya bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambaye naye ameibuka mshindi kwenye uchaguzi mdogo Jimbo la Siha mkoani Kilimanjaro.