Jumatatu , 18th Dec , 2017

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP Simon Sirro amesema Jeshi lake limeongeza nguvu ya ziada ya kupambana na uhalifu nchini hasa kwenye maeneo ya mipakani.

IGP Sirro ameyasema hayo leo mbele ya wananchi wa Wilaya ya Tunduma ambao walisimamisha msafara wake wakati akitokea mkoani Rukwa kurejea Jijini Dar es Salaam.

Mkuu huyo wa Jeshi la Polisi amesema wamefanya hivyo kutokana na maeneo hayo kuonekana kuwa korofi kwa usalama wa raia hivyo wao kama Jeshi la polisi wana dhamana ya kuhakikishia wanaondoa hali hiyo kwa kuongeza nguvu zaidi.

Kwa upande wao wananchi wamepongeza jitihada mbalimbali za Jeshi hilo katika kulinda usalama wao. Pia wameeleza kufurahishwa na kitendo cha IGP Sirro, kusimamisha msafara wake na kwenda kuwasalimia.

IGP Sirro amemaliza ziara yake ya kikazi katika mikoa ya Kigoma, Tabora, Katavi na Rukwa ambapo mbali na shughuli zingine pia amekagua kambi mbalimbali za wakimbizi katika mikoa ya mipakani.