Jumatatu , 18th Dec , 2017

Mbunge wa Tarime Vijijini John Heche (CHADEMA) amedai kwamba Serikali ya CCM haijawahi kupingana na rushwa kwani rushwa zote zinazofanyika zimeasisiwa na Chama Cha Mapinduzi na kwamba wanaonekana kushughulikiwa ni wale wasitakiwa na mfumo.

Heche ameongeza kwamba vita ya rushwa inayozungumzwa na CCM ni vita dhidi ya watu wasiotakiwa na mfumo ndio maana hata kwenye tuhuma za Escrow walikatwa wawili tu japo walitajwa wengi.

Heche amefunguka hayo baada ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kutupilia mbali ushahidi wa 'video clip' iliyowasilishwa ofisini kwao na Wabunge wa CHADEMA, Joshua Nassari wa Arumeru Mashariki pamoja na Godbless Lema wa Arusha Mjini uliokuwa ukidaiwa kuonyesha madiwani wakipokea rushwa kutoka kwa aliyekuwa Mkuu wa Wilaya wa Arumeru .

"Serikali ya ccm haijawahi kupiga vita rushwa na haiwezi kwasababu rushwa zote katika nchi hii zimeasisiwa na zinatokana na ccm, kinachofanyika sasa ni vita dhidi ya watu wasiotakiwa na mfumo, ndio maana hata Escrow waliokamatwa ni wawili lakini bunge lilitaja wengi" .

Takukuru jana walisema kwamba sababu za kutupilia mbali ushahidi wa Wabunge hao ni kutokana na kuharibu ushahidi kwa kuingiza siasa.

Oktoba 2,  2017 Wabunge Joshua Nassari na Godbless Lema walipeleka ushahidi unaodaiwa kuonyesha alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Alexander Mnyeti akiwashawishi madiwani kutoka mkoani Arusha kupokea rushwa ili waweze kujiuzulu nafasi zao.