Jumanne , 4th Jul , 2017

Mkuu wa wilaya ya Kinondoni  Mh.Ally  Happi amegiza jeshi la polisi kumuweka ndani kwa saa 48 Mbunge wa Kawe Mh. Halima Mdee kwa kutoa kauli zinazodaiwa kuwa ni za kumkashifu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli.

Mkuu wa wilaya ya Kinondoni, Ally Happi Kushoto, kulia ni mbunge wa Kawe Halima Mdee

Agizo hilo la Mkuu wa wilaya limekuja leo ikiwa ni siku moja tangu mbunge huyo atoe kauli ya kupingana na Rais John Magufuli kuhusu watoto wanaobeba mimba wasirudi shule aliyoitoa siku chache akiwa mkoani Pwani, huku yeye akimtaka rais afuate sheria na katiba za nchi na kwamba siyo kila kauli yake ni sheria.

Mh. Happi amesema "Mh. Mdee amemtaja kwa jina rais kwamba ana tabia za hovyo, na kwamba tabia zake za hovyo zimempelekea kuona kwamba maneno yake ndiyo sheria ya nchi. Pia amesema kwamba ipo siku rais ataagiza watanzania watembee vifua wazi yaani wanawake kwa wanaume. Nimeshtushwa sana", amesema Mh. Happi .

Hapi ameongeza kwamba maneno aliyoyatoa Mhe. Mdee ni lugha ya matusi yenye lengo la kuleta uchochezi unaoweza kuhatarisha amani na utulivu, hivyo basi yeye kama Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni hatomvumilia mwanasiasa yeyote atakayethubutu kutoa kauli za matusi dhidi ya rais, au zenye kutaka kuleta uchochezi katika wilaya yake.