Jumatano , 27th Apr , 2016

Serikali mkoani Mtwara imesema elimu ya ziada inahitajika kutolewa kwa viongozi katika ngazi za kata, vijiji na vitongoji ili kuwawezesha kutambua majukumu yao na mipaka ya kazi zao.

Mkuu wa wilaya ya Mtwara Fatma Ally

Hayo yameelezwa na Mkuu wa wilaya ya Mtwara Bi. Fatma Ally, wakati wa maafali ya wahitimu wa mafunzo ya mradi wa Elimu na Demokrasia, yaliyoendeshwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania kwa ufadhili wa serikali ya Norway, ambapo amesema viongozi wengi wa ngazi za chini hawajui majukumu yao na hujikuta wanaingilia kazi za wenzao.

Mratibu wa mradi huo ambao unatekelezwa katika halmashauri za wilaya ya Mtwara na ya mji wa Nanyamba ulioanza mwaka 2011, Lucy Agostino, amesema mradi huo unasimamiwa na makatibu wa wilaya kutoka katika vyama vinne vya siasa ambavyo ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Chama cha Wananchi (CUF), Chama cha Mapinduzi (CCM) pamoja na UDP.

Amesema, wahitimu hao 23 waliofanyiwa mahafali ni wahitimu wa awamu ya pili katika mradi huo ambao walianza kupata elimu hiyo mwaka 2012 baada ya wahitimu wa kwanza walioanza kupata elimu mwaka 2011 na kuhitimu mwaka 2014.

Sauti ya Mkuu wa wilaya ya Mtwara Fatma Ally akielezea Elimu ya Majukumu hayo