Jumatatu , 23rd Sep , 2024

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA)imeleta furaha kwa wakazi wa mtaa wa Makurunge, Kata ya Kiluvya wilaya ya Kisarawe baada ya kuanza kutumia maji ya mradi wa uboreshaji huduma ya maji Makurunge wenye thamani ya milioni 72 unaotekelezwa na DAWASA.

Shangwe hiyo imeibuka wakati wa ziara ya Mkuu wa wilaya ya Kisarawe Petro Magoti alipotembelea maeneo ya mradi vikiwemo vizimba vya maji vilivyopo katika vitongoji vya Majumba Sita, Mwanakondoo, Kwa Masista na Tondoroni.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Mhe. Petro Magoti amesema kuwa amefurahishwa na juhudi na utendaji uliofanywa na DAWASA katika kipindi cha muda mfupi na kuhakikisha wakazi wa Makurunge wanapata maji kwa urahisi na kwa karibu.

Aidha Mhe. Magoti amewataka wakazi wa Mtaa wa Makurunge kulinda miundombinu hiyo ya maji ili isiharibiwe na watu wasio na mapenzi mema na kuwataka kutoa taarifa kwa vyombo vya usalama ili kuwachukulia hatua waharibifu watakaobainika.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa DAWASA Bw. Paul Sulley ameeleza kuwa mradi huo wa uboreshaji huduma ya maji Makurunge umegharimu milioni 72 kwa kuhusisha kutengeneza chanzo cha Maji ya DAWASA kutoka kwenye mtandao wa kisima ya RUWASA, Ulazaji wa mabimba ya inchi 4 kwa kilometa 12, utoaji na ufungaji pampu ya kupeleka maji kwenye tanki la Majumbasita pamoja na Ukatabati wa vizimba vinne na vingine vipya ikiwa ni jitihada za Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.