Ijumaa , 16th Feb , 2018

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimekanusha taarifa zinazosambaa mitandaoni kuwa imejitoa katika uchaguzi mdogo wa marudio kwenye jimbo la Kinondoni, Siha na kata nane nchini na kuwataka wananchi kuzipuuza taarifa hizo wazipatapo.

Akizungumza na mwandishi wa EATV,  Mkurugenzi wa Itikadi, Mawasiliano na Mambo ya Nje- CHADEMA John Mrema amesema kuwa taarifa hizo hazina ukweli wowote na kudai wanaofanya hivyo ni kundi cha watu wachache wenye lengo la kutaka kupotosha umma ili kesho wasiende kupiga kura.

"Taarifa hizo ni za uongo zinasambazwa na watu ambao wameshashindwa naomba watu wazipuuze. Tunapozungumza sasa hivi Mwenyekiti wa chama Mhe. Mbowe anahitimisha kampeni katika jimbo la Kinondoni na Mhe. Lowassa yupo kule Siha nae anahitimisha kampeni",amesema Mrema.

Pamoja na hayo, Mrema ameendelea kwa kusema "tunaomba kuwaambia wananchi na wanachama wa CHADEMA kuwa hiyo sio barua yetu na pia sio utaratibu kwa mujibu wa kanuni mwenyekiti wa chama kuandika barua ya kujitoa kama mtu mwenye haki ya kujitoa ni mgombea. Kwa hiyo hata hao watu walioandika hiyo barua hawajui sheria za uchaguzi zinasemaje".

Kwa upande mwingine, Mrema amezidi kuwasisitizia wananchi kuzipuuza taarifa zozote zinazotoka sasa kuhusu kutoshiriki uchaguzi huku akiwaomba wananchi katika Jimbo la Kinondoni na Siha kujitokeza kwa wingi kesho kushiriki kupiga kura kwa sababu ni haki yao ya msingi.