Jumamosi , 27th Jul , 2024

Rehema Paulo (26) Mkazi wa kata ya Katente iliyopo wilaya ya Bukombe mkoani Geita amejeruhiwa kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali sehemu za kichwani na kukatwa viganja huku chanzo kikitajwa kuwa ni wivu wa mapenzi.

 

Tukio hilo limetokea Julai 24, 2024 ambapo inadaiwa mwanamke huyo alikuwa na mgogoro wa kimapenzi na mwanaume aliyefahamika kwa jina la Baba Law na kuwa siku ya tukio, alipigiwa simu na mtu wakaonane na alipofika, alivamiwa na kujeruhiwa.

“Nilipigiwa simu majira ya saa tano usiku na mwenyekiti maana mimi ni katibu wa balozi kwamba rehema amekatwa mapanga nikauliza rehema gani tena wakaniambia yule anayeuza sokoni amekatwa akiwa sokoni nikaamua nimpigie mwenyekiti tukaamua tupande bodaboda mpaka hospitali tukakuta kweli amelazwa hospitali hali yake ikiwa mbaya kwasababu amejeruhiwa kichwani na kukatwa mikono yote miwili” amesema Joyce Silenda ambaye ni Katibu wa balozi

“Nilipigiwa simu na raia mwema akaniambia dada yako amekatwa mikono nikakimbia kufika eneo la tukio nikakuta ni kweli ninaomba jeshi la polisi litusaidie kuwakamata walio husika na tukio hilo maana ndugu yetu hali yake ni mbaya anahisi maumivu makali sana”Gaudensia George - Ndugu wa aliyejeruhiwa

“Nikweli alifikishwa hapa hospitali tulimpatia huduma ya kwanza na kumshona sehemu alipojeruhiwa lakini viganja vimehifadhiwa mochwari kwaajili ya kusubiri utaratibu wa familia kuvihifadhi kwa mujibu wa taratibu zao” Deograsia Mkapa - Mganga mkuu  halmashauri ya wilaya Bukombe

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita SACP Safia Jongo amethibitisha kutokea kwa mkasa huo huku akisema kuwa hadi sasa mtuhumiwa na mke wake wametoroka na wanasakwa huku akiitaka jamii kupunguza roho za visasi 

“Hadi sasa Baba Law na mke wake wametoroka nyumbani na Jeshi la Polisi linaendelea kufuatilia ili kumkamata Lakini matukio yanayotokea  yanasababishwa na wananchi kulipiziana visasi na kujichukulia sheria mkononi niwaombe  wazazi kuwalinda watoto na mnapoona mmekwama ni vizuri mkaomba msaada ustawi wa jamii ili mtatuliwe changamoto zenu” SACP Safia Jongo -RPC Mkoa wa Geita