Jumatano , 28th Apr , 2021

Serikali imeombwa kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara kutoa vibali na kutengeneza mazingira ya wafanyabiashara wa mahindi kuuza katika masoko ya nje ambayo yameonyesha uhitaji mkubwa tofauti na ilivyo sasa wengine hupitisha kwa njia za panya.

Gari likiwa na shehena ya Mahindi.

Mapema hii leo EATV imetemblea katika masoko kadhaa ya nafaka na kuzungumza na wafanyabiashara wa mahindi ambao wameiomba serikali kutumia mabalozi wake kwenye nchi za nje kupata vibali vya mmoja kwa moja kupeleka bidhaa hiyo.

" Mimi niiombe Serikali ama waziri mwenye dhamana ya Viwanda na Biashara kutizama upya sera ya kama kuna Soko la nje mahala fulani tuwatumie  Mabalozi wetu kupata masoko ya mazao yetu sasa hivi mahindi yanahitajika sio Kenya tuu", amesema Tanda.

Aidha wameeleza jinsi hali ilivyo kwa sasa katika Soko la ndani ambapo mahindi huuzwa kilo kwa shilingi 400 hali inayofanywa mkulima kijijini kuuza mahindi hayo kwa hasara zaidi.

Sambamba na hilo wameomba Wizara ya Viwanda na Biashara  kuandaa  safari za nje kwa wafanyabiashara kujifunza fursa zaidi kwa wenzao kutoka mataifa mbalimbali kuona wao wanafanyaje.