Thursday , 12th Jun , 2025

Ndege ya India, Air India, iliyokuwa inaelekea London ikiwa na abiria 242 imeanguka dakika chache tu baada ya kupaa kutoka mji wa magharibi mwa India wa Ahmedabad 

Haya yamethibitishwa na shirika hilo la ndege na polisi ya nchi hiyo, bila kuweka wazi iwapo kulikuwa na maafa.
Ndege hiyo ilikuwa inaelekea uwanja wa ndege wa Gatwick nchini Uingereza na maafisa wa polisi wamesema imeanguka katika eneo la makaazi ya watu karibu na uwanja wa ndege.

Waziri Mkuu wa India Narendra Modi amesema ameshtushwa sana na ajali hiyo ya ndege.

Mtandao wa kufuatilia safari za ndege wa Flightradar24 umesema ndege hiyo ilikuwa aina ya Boeing 787-8 Dreamliner, mojawapo ya ndege za kisasa zaidi zinazotumika.

Mojawapo ya kituo cha televisheni nchini India kimeionyesha ndege hiyo ikipaa juu ya eneo la makaazi ya watu kisha ikapotea kabla kuzuka kwa moto mkubwa ulioonekana angani kutoka eneo hilo lenye nyumba za makaazi.
Baadhi ya video zimeonyesha watu wakiondolewa eneo la tukio na vitanda vya magurudumu na kupelekwa katika ambyulensi.

Kulingana na kituo cha kuongoza ndege katika uwanja wa ndege wa Ahmedabad, ndege hiyo ilipaa mwendo wa saa saba na dakika thelathini na tisa kutoka barabara ya ndege ya 23. Ilipiga simu kuashiria dharura dakika chache baadae ila hakukuwa na mawasiliano zaidi kutoka ndegeni humo.

Mara ya mwisho ndege kuanguka nchini India, ilihusisha ndege ya Air India Express mwaka 2020, ambayo ni tawi la bei nafuu la shirika la Air India na watu 21 walifariki dunia katika tukio hilo.