Wednesday , 28th Aug , 2024

Mahakama Kuu ya Tanzania masijala ndogo ya Dar es Salaam, imetupilia mbali kesi namba 23998, ya madai ya Deusdedith Soka na wenzie dhidi ya IGP, AG,DPP,DZPC,ZCO,OCCID TEMEKE, OCS TEMEKE, inayohusu kuwashikilia viongozi wa BAVICHA wilaya ya Temeke.

Baadhi ya watu waliojitokeza kusikiliza Kesi ya Mwenyekiti BAVICHA wilaya ya Temeke na wenzie watatu.

Shauri hilo limetupiliwa mbali leo hii Agosti 28, 2024 baada ya Mahakama kutoridhishwa na vielelezo vya ushahidi uliopelekwa Mahakani hapo na jopo la Mawakili likiongozwa na Peter Madeleka.

Shauri hilo ni kuhusu viongozi wa BAVICHA wilaya yav Temeke ambao walikamatwa na kupelekwa kituo cha polisi Chang'ombe Agosti 18, 2024 ambapo ni siku 10 zimepita toka vijana hao watatu wakamatwe bila kufahamika walipo.

Viongozi hao wanaodaiwa kuweka kizuizini ni Mwenyekiti wa Wilaya ya Temeke, Deusdedith Soka na Katibu wake, Jacob Mlay pamoja dereva wao wa pikipiki, Frank Mbise, ambao wanadaiwa kukamatwa na Polisi katika kituo cha Polisi Chang'ombe, Temeke tangu Agosti 18, 2024.

Baada ya maamuzi hayo ya Mahakama Jopo la Mawakili limesema litakata rufaa ili kupata haki ya viongozi hao wa Bavicha ambao hawajulikani walipo.

Aidha Mahakama imeliamuru Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi na kuwatafuta viongozi hao  wa BAVICHA , ambao hawajulikani walipo.