
Askofu Dkt Getrude Rwakatare, wakati wa uhai wake.
Kwa mujibu wa Spika Ndugai, mazishi ya Mama Rwakatare, yatasimamiwa na Serikali na kuhudhuriwa na watu wachache ambao hawatazidi 10.
Mama Rwakatare amefariki Dunia Aprili 20, 2020, katika hospitali ya Rabininsia jijini Dar es Salaam, alikokuwa akipatiwa matibabu, ambapo kwa mujibu wa mwanaye Mutta Rwakatare, alisema kuwa Mama yao alikuwa akisumbuliwa na tatizo la moyo na presha.
Mama Rwakatare alizaliwa Disemba 31, 1950, hivyo amefariki akiwa na umri wa miaka 70, ikumbukwe kuwa aliwahi kuhudumu katika nafasi mbalimbali za uongozi, ikiwemo Ubunge wa Viti Maalum wa CCM Mvomero na Mbunge wa kuteuliwa na Rais wa Awamu ya Nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete.
Aidha mnamo mwaka 1987 Mama Rwakatare alianzisha Shule za St.Marys, kuanzia ngazi ya awali, Msingi na Sekondari, ambapo baadaye mwaka 2006, alianzisha kituo cha watoto yatima alichokiita kwa jina la Bright Future.