Ijumaa , 30th Mei , 2025

Kuelekea mchezo wa fainali Ligi ya mabingwa barani Ulaya (UEFA Champions League) kati ya kikosi cha PSG dhidi ya Inter Milan, István Kovács raia wa Romania ameteuliwa kusimamia sheria 17 za soka huko mjini Munich hapo kesho majira ya Saa nne kamili usiku.

István Kovács

Miezi kumi na miwili iliyopita, Mromania huyo alichezesha mchezo wa fainali UEFA Europa League huko Dublin ambao Atalanta walishinda 3-0 dhidi ya Bayer Leverkusen na kabla ya fainali hiyo alipata kuchezesha mechi mbili za michuano ya EURO 2024. 

István uhodari wake wa kumudu mchezo, umemfanya kuteuliwa na UEFA kuchezesha fainali hiyo Jumamosi na kuwa mtu wa kwanza kuchezesha fainali za michuano mikubwa ya UEFA ngazi ya klabu, baada ya kuchezesha fainali ya kwanza ya UEFA Conference League mwaka wa 2022 bingwa akiwa AS Roma kwa goli 1-0 dhidi ya Feyenood. 

Mromania huyo mwenye umri wa miaka 40, amesema kuwa amejipa muda zaidi wa utayari wake kuelekea mchezo huo ''Mchana nitapata chakula, na baada ya hapo nitalala kwa saa moja hadi mbili. Saa tatu kabla ya mchezo, nitasikiliza muziki fulani, kuoga na kisha nitakuwa tayari kwenda uwanjani.''- István Kovács