Thursday , 17th Nov , 2016

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ametia saini Sheria ya Huduma za Habari ya Mwaka 2016 iliyopitishwa na Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkutano wake wa 5 Mjini Dodoma.

Rais Magufuli

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais katika taarifa yake kwa vyombo vya habari imesema kuwa Rais Magufuli amesaini Sheria hiyo jana tarehe 16 Novemba, 2016.

Taarifa hiyo imesema pia kuwa Dkt. Magufuli amewapongeza wadau wote kwa kufanikisha kutungwa kwa Sheria hiyo.

"Naamini kuwa Sheria hii itasaidia kuboresha sekta ya habari kwa manufaa ya wanataaluma wenyewe na Taifa" amesema Rais Magufuli.

Mnamo Novemba 04, mwaka huu, wakati Rais Magufuli akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari, aliahidi kuusaini muswada huo mara moja utakapomfikia huku akiusifia kuwa ni sheria nzuri inayolenga kulinda maslahi ya waandishi wa habari na kuweka heshima katika tasnia hiyo.