Friday , 1st Jul , 2016

Timu ya taifa ya Ureno imetinga hatua ya nusu fainali katika michuano ya Euro 2016 inayoendelea nchini Ufaransa na kuwa nchi ya kwanza kufuzu katika hatua hiyo baada ya kuifunga Poland kwa mikwaju ya penalti 5-3.

Katika mchezo huo Poland ilifanikiwa kuandika goli la kwanza mapema kipindi cha kwanza katika dakika ya tatu ya mchezo kupitia mchezaji wao Robert Lewandowski kabla ya Renato Sanches kuisawazishia timu yake ya Ureno.

Hadi dakika 120 za mchezo huo zilishuhudiwa timu hizo zikiishia kwa sare ya goli 1-1.

Mreno Ricardo Quaresma alikuwa shujaa kwa timu yake baada ya kupiga penalti ya mwisho iliyoivusha katika hatua nyingine huku kiungo wa Jakub Blaszczykowski akikosa mkwaju wa penalti kwa upande wa Poland.

Ureno itakutana katika hatua ya nusu fainali na mshindi wa mchezo kati ya Wales na Ubelgiji.