Thursday , 25th Apr , 2019

Klabu ya soka ya KMC, leo inashuka kwenye uwanja wake wa nyumbani wa CCM Kirumba, kuikaribisha Simba ambapo katika mchezo huo KMC itakuwa bila ya kinara wake wa magoli Emmanuel Mvuyekure.

Emmanuel Mvuyekure mwenye jezi namba 10 mgongoni.

Afisa habari wa KMC, Anwar Binde ameithibitishia www.eatv.tv kuwa mshambuliaji wao huyo raia wa Burundi hatakuwa sehemu ya mchezo wa leo kutokana na kuumia mazoezini.

''Ni kweli Mvuyekure anakosekana leo, sababu ni kwamba aliumia kwenye maandalizi ya mchezo huo''. amesema Binde.

Mvuyekure mpaka sasa ana magoli 8 na ndiye kinara wa mabao ndani ya kikosi hicho kwenye ligi kuu soka Tanzania Bara.

Idadi ya mabao ya Mvuyekure ni nusu ya yale ya mshambuliaji wa Simba Meddie Kagere, ambaye mpaka sasa ana mabao 16.

Katika mchezo wa kwanza uliopigwa kwenye uwanja wa taifa jijini Dar es salaam, Simba iliibuka na ushindi wa mabao 2-1. 

Simba ipo nafasi ya 3 kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 63 kwenye mechi 25, wakati KMC ikiwa katika nafasi ya 7 na pointi 42 katika mechi 32.