Saturday , 16th Jun , 2018

Mkuu wa Habari na Mawasiliano wa Mabingwa wa Ligi Kuu (VPL) Simba SC, Haji Manara amefunguka na kumwagia sifa nyota wa timu ya Taifa ya Ureno, Cristiano Ronaldo huku akidai mchezaji huyo ndio mtu maarufu ulimwenguni kote na mtu pekee aliyepigwa picha nyingi tokea alipoumbwa Adam na Hawa.

Manara ametoa kauli hiyo asubuhi ya leo Juni 16, 2018 baada ya Ronaldo kuingia kwenye 'record' ya kuwa mfungaji wa kwanza kufunga Hat- Trick ya kwanza katika fainali za Kombe la Dunia 2018 kwenye mechi ya Kundi B iliyowakutanisha Ureno dhidi ya Hispania.
 
"Kuna mamilioni ya watu wanaocheza soka kote duniani lakini mchezaji bora ni mmoja tu, Cristiano Ronaldo ndio mwanadamu maarufu kupita wote ulimwenguni na ndio mtu aliopigwa picha nyingi kupita wote toka alipoumbwa Adam na Hawa", amesema Manara.

Pamoja na hayo, Manara ameendelea kwa kusema "hata mitandaoni yeye ndio anaongoza kwa 'followers' kuliko kiumbe chochote kilicho hai chini ya jua, mchukie utakavyo ila huyo ndio Cristiano Ronaldo ama 'De le boss wa Portugal".

Cristiano Ronaldo ni mchezaji wa tatu wa Ureno kufunga Hat -Trick katika michuano ya Kombe la Dunia nyuma ya Eusebio na Pauleta ambapo pia Hat -Trick hiyo ni ya sita kwa timu ya Taifa ya Ureno.