Monday , 16th Feb , 2015

Nchi za Ethiopia, Somalia na Djibout ambazo zilikuwa zishiriki katika michuano ya mpira wa wavu wa Ufukweni kanda ya tano zimeshindwa kushiriki michuano hiyo kutokana na kukosa fedha za maandalizi ya michuano hiyo.

Akizungumza na East Africa Radio, Mwenyekiti wa Chama cha wavu nchini TAVA, Augustino Agapa amesema, michuano hiyo iliyoanza leo ilitakiwa kushirikisha nchi sita ambapo hivi sasa nchi zilizobakia katika ushiriki huo ni wenyeji Tanzania, Burundi an Kenya ambapo timu mbili zitakazofanya vizuri zitafuzu kuingia mzunguko wa pili kushindana na kanda nyingine za Afrika ambapo zikifanya vizuri zitaweza kushiriki michuano ya Olimpiki Brazili mwaka 2016.

Agapa amesema, licha ya timu kuwa pungufu katika michuano hiyo, ratiba ya michuano hiyo itaendelea kama kawaida ambapo watanzania wametakiwa kujitokeza katika kuusapoti mchezo huo ambao ni muhimu na unazidi kufanya vizuri hapa nchini.